Friday, 3 March 2017
JIFUNZE NAMNA YA KUULINDA MOYO WAKO(AU NAFSI) NA KUUTOA KWENYE MAANGAMIZO
*Na Mwl Mwakatwila*
Bwana Yesu Kristo asifiwe sana wana darasa wote!!! Namshukuru Mungu ambaye amenipa muda huu ambao nami nimeona niutumie kukuletea somo darasani.
đŸ‘‰Kabla sijakuletea somo leo hii nipo na mambo mawili ya kukushirikisha.
1.Napenda kuwashukuru wote walionitakia sikukuu ya kuzaliwa kwangu jana tar 2 March. Mungu awabariki sana na asante kwa maombi yenu na faraha yenu kwetu. Tunahitaji maombi yenu sana, msikome kutuombea kwa Mungu.
2.ninapenda kukupa taarifa kuwa tar *5-12 March 2017* *kila siku saa tisa hadi saa kumi na mbili na nusu jion* tutakuwa na semina pale Betheki Sae KKKT (Mbeya karibu na Sae mitamboni Tanesco) mkaribishe na ndugu yako na rafiki yako.
✨Katika kipindi kilichopita nilikufundisha namna unavyoweza kuanza kuihuisha nafsi yako kwa kutumia neno la Mungu.
Ebu tuendelee kidogo kwenye eneo hilo hilo. Mungu alilileta neno lake kwa makusudi kabisa ya kuijenga upya nafsi au moyo wa mwanadamu baada ya kuharibiwa na shetani pale bustanini Edeni. Nafsi ya mtu ili poteza uzima wake baada ya dhambi kuingia. Sikia hii habari ya mtu kuwa na uchungu, wivu, uzinzi, kuwa na mazingira ya makuzi mabaya, kuabudu sanamu, Kutosamehe nk ,ni matokeo ya uasi uliofanyika pale bustanini Edeni.
Kwa ufupi nikwambie. Dhambi ilipoingia tu, ndiyo ikawa sumu ya kuiangamiiza nafsi ya mtu. Akili zikawa mbaya yaani mfumo wa kuwaza na kufikiri wa mtu ukawa mbaya. Mungu ili aihuishe hiyo nafsi ya mtu iliyoharibiwa na dhambi akaamua kuleta *DAWA YA KUIPONYA HIYO NAFSI NAYO INATWA NENO.*
Najua haraka haraka umewaza kuwa Bwana Yesu ndiye mponyaji wa mioyo yetu. Na umewaza kuwa ntamuomba Bwana Yesu ili auponye moyo wangu basi. Sikia nikwambie. Huyo Bwana Yesu unayeenda kumuomba ndiye Neno. Ukimuomba niponye moyo wangu atakachokifanya *ATAKUJA KAMA NENO.*
Usipompokea kama neno usitegemee uponyaji wowote moyoni mwako. Ukimuomba Mungu niponye moyo wangu au niuhishe moyo wangu fahamu atatuma neno. Angalia mistari hii. "Nafsi zao zachukia kila namna ya chakula, Wameyakaribia malango ya mauti.Wakamlilia BWANA katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao. Hulituma neno lake, huwaponya, Huwatoa katika maangamizo yao."(Zaburi 7:18-20)
Nafsi yako ikiwa imepigwa, hata chakula huwezi kula,Yaani umeumizwa moyoni wee hata njaa huisikii na unaona kabisa moyo wako umeangamia , mfumo wa akili zako umekufa, yaani huna wazo na fikra nzuri. Unawaza teso lako tuu. Na umeanza kuomba Mungu aiponye nafsi yako. Fahamu atakachokifanya ATAKULETEA NENO. Ukilisikia hilo neno na kuliweka kwenye matendo ndipo uponyaji wa moyo wako hutokea.
Sikia. Kwa lugha nzuri niseme atakupa utaratibu au agizo furani ulifanye ili uwe na uzima huko moyoni mwako. Ndani ya neno la Mungu kumewekwa utaratibu. Kwa lugha nzuri tunaita sheria au amri. Kwa lugha nzuri sana ya kueleweka tunaita maagizo. Ngoja kidogo nikupe mfano huu. Ukiugua leo hii na ukaenda hospitali utakutana na wataalamu. Wataalamu hao watakuambia kisa au kiini cha ugonjwa wako ninini, na watakupa maagizo au utaratibu au amri ya nini ufanye ili uwe mzima.
Watakuagiza au kukupa amri kama hii. Kunywa dawa hizi vidonge viwili kwa siku mara tatu. Hilo ni agizo au ni utaratibu au amri au sheria ya uponyaji wako. Usipotii utaratibu huo nakwambia ukweli usitegemee kupona. Sasa turudi kwa Mungu pia kama daktari wa mioyo au nafsi zetu. Pia naye alipogundua kuwa mtu ana moyo uliobeba ugonjwa wa kufisha. Akaamua kuuponya huo moyo wa mtu.
Akampa utaratibu au sheria au maagizo maalumu ili huyo mtu aanze kuufanya ili aiponye nafsi au moyo wa mtu uliougua au kushambuliwa na shetani. *AKAMPA DAWA IITWAYO NENO LA MUNGU*.
Sikiliza maneno haya uone hiki ninachokuambia. " Mwanangu, usiisahau sheria yangu, Bali moyo wako uzishike amri zangu. Maana zitakuongezea wingi wa siku. Na miaka ya uzima, na amani. Rehema na kweli zisifarakane nawe; Zifunge shingoni mwako; Ziandike juu ya kibao cha moyo wako.Ndivyo utakavyopata kibali na akili nzuri, Mbele za Mungu na mbele ya mwanadamu........Basi yatakuwa uzima kwa nafsi yako, Na neema shingoni mwako.."(Mithali 3: 1-4 na ule wa 22)
Ukiipitia mistari hiyo utaona wazi kuwa. Ili nafsi ya mtu iwe na uzima inatakiwa huyo mtu aisikie sheria au amri au utaratibu au maagizo yatokayo kinywani mwa Mungu tunaita NENO LA MUNGU. Ukipitia hiyo mistari utaona ili mtu awe na akili nzuri maana yake ziliharibika au zilikua ngonjwa, ehehee!!! Anatakiwa huyo mtu aisikie sheria au amri au utaratibu au maagizo yatokayo kinywani mwa Mungu tunaita NENO LA MUNGU.
Kumbuka ndani ya moyo huko ndiko kuna akili. Chanzo cha akili au ufahamu kinaanzia kwenye milango mitano ya ufahamu, macho kuona ,pua kunusa, ulimi kuonja,masikio kusika na kukugusa. Milango hiyo mitano ikifanya kazi yake huko ndani ya moyo kunatokea wazo, wazo linazaa fikra fikra inazaa kutafakali na ndipo mtu anapata kitu ufahamu au kujua au ujuzi tunaita akili.
Sasa sikia. Mungu aligundua mfumo mzima wa milango ya ufahamu wa mtu na mfumo mzimaa wa moyo wa mtu huko ndani ni mgonjwa yaani kuanzia mawazo yake hisia zake utashi wake akaamua kuutengenezea dawa na dawa hiyo IMEBEBA NDANI YA NENO LAKE.
Sikia kila agizo alilokupa Mungu lililo ndani ya neno lake KAZI YAKE NI KUIPONYA NAFSI AU MOYO WAKO. Mimi nakwambia ukitaka leo wingi wa siku yaa ni uwe hai anasema sikiliza maagizo yake. Mfano unataka akili nzuri yaani uwe na ufahamu mkubwa anasema sikiliza neno lake. Tatizo lipo hapa. Watoto wa Mungu wengi sana wana Biblia na wanasikia sana agizo kutoka kwa Mungu ILA WENGI HAWAYAWEKI KWENYE MATENDO YALE WALIOAGIZWA.
Fikiria daktari kakuambia kunywa kidonge kimoja asubuhi na jioni. Wewe unakunywa jioni tu asubuhi hunywi unategemea kupona? Ndivyo ilivyo. Fikiria kidogo, watu wengi hujaa makanisani kila wiki. Wewe waulize MMEENDA KULE KUFANYA NINI? Unabeba Biblia ili upate nini? Unasoma neno la Mungu na kusikiliza redio mafundisho au kwenye Tv, nk ILI UPATE NINI?
Jibu la wengi utasikia nipate uzima. Muulize uzima upi? Wengi utasikia wa milele!! Utapataje uzima huo wakati hunywi dawa? Ngoja niseme kitu cha ajabu kidogo. Utaupataje uzima wa milele wakati AKILI ZAKO TU NI NGONJWA? Wewe wafuatilie watu wengi waliokoka utagundua ninachokuambia. YAANI WENGI SANA WAMEHIFADHI MANENO YA MUNGU KWENYE MAKARATASI LAKINI SI MOYONI!!!
Kila siku unasoma maandiko kama hadithi. Husomi kama TIBA YA NAFSI YAKO. Mimi nakwambia wote tutaenda kanisani ila usifikiri wote tunapokea maagizo kutoka kwa Mungu sawasawa. Wengi huenda kusikiliza maagizo hayo na wanayaacha kanisani mlemle!!! Ngoja nikupe mfano. Wewe leo hii unataka uzima wa milele. Maagizo ya uzima wa yanasema. "Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu. Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu. [Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina.]"(Mathayo 6:12-13).
Sikia ili nafsi yako ipate uzima wa milele lazima USAMEHEWE DHAMBI ZAKO. Kitakachotupeleka mbinguni ni msamaha tuupatao kutoka kwa Mungu kwa kupitia Bwana Yesu Kristo Wala si kitu kingine. Sasa sikia. Mtoa msamaha au daktari katupa dawa maalumu ya sisi tutakao uzima huo wa milele. Kasema wasameeni waliowakosea na ndipo na mimi nawasamehe nyinyi.
Sasa nenda huko makanisani, kaangalie wagonjwa wamuendeao Daktari ili awape uzima. Utashanga kila siku wanapewa dawa hiyo inaitwa SAMEHE. Na wainywe SABA MARA SABINI ili wapate uzima wa milele. Utashangaaa WENGI HAWANYWI ILA WANAVISINGIZIO VINGIIIII WEEE!!! Hoo unajua daktari kidonge hiki hakiwezekani kumeza kichungu nk!!! Sikia USIPOKINYWA UTAKUFA NA DHAMBI ZAKO.
Mimi nawaambia ukweli. Kama leo hii hutaki majaribu. Daktari kasema ombeni msiingie majaribuni. Swali langu kwako umekunywa hiyo dawa leo ya kukuzuilia wewe majaribu, yaani umetii hilo neno leo umeomba usiingie majaribuni? Kama hauja fanya unategemea nini sasa?
Mungu anatupa agizo anasema hivi. "Mwe na hasira, ila msitende dhambi; jua lisichwe na uchungu wenu bado haujawatoka; wala msimpe Ibilisi nafasi."(Waefeso 4:26-27). Kama wewe leo hii hutaki kumpa ibilisi nafasi huko ndani ya moyo wako, au kwenye nyumba yako, au kwenye akili zako au kwenye mwili wako Mungu kakupa dawa. Anasema UWE NA HASIRA ILA USITENDE DHAMBI. Dhambi ipi ?
Anasema USIUKALISHE UCHUNGU MPAKA JUA KUCHWA. Fikiria leo hii una bp na unataka Mungu akuponye unafikiri atakupa dawa gani? Atakwambia ONDOA UCHUNGU. Ibirisi anapata nafasi ya kuwatesa watu wengi mno kwa KUPITIA HASIRA IZAAYO UCHUNGU.
Maandiko yanasema Usifanye haraka kukasirika moyoni. Wewe huliweki hilo neno kwenye matendo, wakikuudhi kidogo tu HASIRA ZIMEWAKA. Nakwambia ukweli kadri unavyokasirika hovyo hovyo ndivyo unampa ibirisi nafasi ya KUUPIGA MFUMO MZIMA WA AKILI YAKO. Huwezi waza mambo mengine ukiwa na hasira na uchungu. Na shetani akikukuta wewe ni mtu wa namna hiyo nakwambia atakutesa sana.
Nataka ujifunze kutafuta utaratibu wa kuiponya nafsi ibebayo hasira. Nenda kwenye neno la Mungu. Utaona huko ndani Unaagizwa USIFANYE HARAKA KUKASIRIKA. Kama unauchungu nenda kwenye neno utaona lina kuambia usiukalishe uchungu mpaka jua kuchwa. Ili uwe na AMANI NA WATU WOTEEE NI KAZIMA UJIFUNZE KUWASAMEHEEE. Na usiposamehee fahamu hupewi msamaha na Mungu.
Naamini umenielewa kwa leo. Ebu ITIBU HIYO NAFSI YAKO KWA KUPITIA NENO. Kama leo una hasira tafuta mistari yote ndani ya maandiko inayozungumzia hasira ilishe nafsi yako, tafakari hilo neno UTAPATA AKILI NZURI YA KUJUA KUWA HASIRA HUKAA KIFUANI MWA WAPUMBAVU." Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, Maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu"(Mithari7:9)
Na wewe hufai kabisaa kuwa mpumbavu wewe NI MTOTO WA MUNGU. ITIBU HIYO NAFSI YAKO KWA KUTUMIA NENO TENDEA KAZI YOTE UNAYOFUNDISHWA NDIPO UTAKUA NA AKILI NZURI NA UZIMA MOYONI MWAKO. Mungu akubariki sana
Wako
Mr Steven & Mrs Beth Mwakatwila
www.mwakatwila.org
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment